Titani (kutoka Kigiriki: Τῑτάν) ni mmojawapo kati ya miezi ya sayari Zohali wenye ukubwa wa sayari ndogo.
Kipenyo chake kwenye ikweta ni kilomita 5,150 na inasogea kwenye mzingo wenye umbali wa kilomita 1,221,865 km kutoka Zohali. Titani ilitambuliwa mwaka 1655 na mwanaastronomia Christiaan Huygens kwa kutumia moja ya darubini za kwanza iliyoboreshwa. Titani ni mwezi mkubwa wa Zohali na mwezi mkubwa wa pili katika mfumo wa Jua letu. Hata ni kubwa kuliko sayari Utaridi.
Zamani Titani ilikadiriwa kuwa mwezi mkubwa katika mfumo wa jua. Lakini safari ya Voyager 1 ilipita Titani mwaka 1979 na vipimo vya kipimaanga hicho vilionyesha ya kwamba uso wa Titani unafichwa na angahewa zito lenye unene wa kilomita 900 . Kwa hiyo imejulikana ya kwamba Ganymedi, mwezi wa Mshtarii, ni kubwa zaidi.
Ikiwa Titanii ni kubwa kushinda Utaridi inajulikana ya kwamba masi yake ni ndogo. Kwa hiyo inaaminiwa ya kwamba unaundwa hasa na barafu ya maji. Hata uso wa mwezi ni hasa barafu ya maji ambayo ni imara kama mwamba kutokana na baridi kali ya 180 C° usoni mwake. Chini ya ganda imara hilo kuna uwezekano wa kuwa na bahari ya maji.
Kiini cha Titani ni silikati na metali. Graviti ya Titani ni ndogo; mtu anayeweza kuruka mita 1 juu ya uso wa dunia angeweza kuruka mita 7 juu ya uso wa Titani.
Titani inapita obiti yake katika siku 15 na saa 22 ikizunguka sayari yake Zohali mara moja. Muda huo unalingana na mzunguko wa Zohali kwenye mhimili wake au muda wa siku 1 ya Zohali.
Mzingo wa Titani unafanana na duara ingawa si duara kamili.
Kigezo:Gallery
Pamoja na Dunia yetu ni mahali pa pekee penye angahewa zito la gesi. Lakini haifai kwa binadamu kwa sababu ni baridi sana na gesi zake ni nitrojeni pamoja na hidrokaboni kama methani. Pamoja na Dunia ni pia mahali pa pekee katika mfumo wa Jua penye maziwa na mito lakini hii si ya maji bali na methani kiowevu.
Angahewa la Titani lina shinikizo mara 1.45 kuliko Dunia; densiti yake ni mara nne densiti ya angahewa la Dunia. Tabia hizo, pamoja na kiwango kidogo cha upepo na graviti iliyo ndogo kuliko duniani, zinaaminiwa kuruhusu upelelezi wa mwezi huo kwa njia ya vyombo vya hewani. Mamlaka ya usafiri wa anga ya Marekani inaandaa mradi wa Dragonfly itakayopeleka helikopta hadi Titani kwenye mwaka 2037.
Tarehe 1 Julai 2004 chombo cha angani Cassini–Huygens iliingia katika mzingo wake kuzunguka Zohali. Sehemu ya Huygens iliachana na Cassini na kufika usoni pa Titani 14 Januari 2005 ambako iliweza kutuma data kwa dakika 72. Data hizo zilihusu zaidi angahewa la mwezi huo na kuwepo kwa viowevu. Cassini inaendelea kuzunguka Titani na Zohali pamoja na miezi mingine ya Zohali. Cassini ilithibitisha kuwepo kwa maziwa makubwa ya hidrokaboni karibu na ncha ya kaskazini. Ziwa kubwa lenye eneo kama Bahari ya Kaspi duniani ilipewa jina la Kraken Mare.
This article uses material from the Wikipedia Kiswahili article Titani (mwezi), which is released under the Creative Commons Attribution-ShareAlike 3.0 license ("CC BY-SA 3.0"); additional terms may apply (view authors). Maudhui yanapatikana kwa chini ya CC BY-SA 4.0 isipokuwa iwe imebainishwa vinginevyo. Images, videos and audio are available under their respective licenses.
®Wikipedia is a registered trademark of the Wiki Foundation, Inc. Wiki Kiswahili (DUHOCTRUNGQUOC.VN) is an independent company and has no affiliation with Wiki Foundation.