Basilika la Mt.
Petro mjini Roma ni kanisa kubwa kuliko yote duniani na linatumiwa sana na Papa, ingawa si Kanisa kuu la jimbo lake.
Basilika hilo lote liko ndani ya eneo la Vatikani ambalo ni dola au nchi huru ndogo iliyoko ndani ya mji wa Roma (makao makuu ya Italia).
Kumbukumbu ya kutabarukiwa kwake inafanyika kila mwaka tarehe 18 Novemba.
Kanisa hili lilianzishwa mnamo mwaka 324 na Kaisari Konstantino Mkuu aliyeagizwa ujenzi mahali ambapo watu waliamini Mtume Petro aliuawa kwa ajili ya imani ya Ukristo akazikwa wakati wa Kaisari Nero (kabla ya mwaka 68).
Kanisa hilo la kale lilionekana bovu wakati wa karne ya 16, hivyo Papa Julius II aliamuru libomolewe ili kujenga kanisa jipya.
Muda wa ujenzi ulikuwa miaka 120: ulianza mwaka 1506 ukakamilishwa mwaka 1626.
Wasanii mashuhuri walishiriki katika ujenzi na upambaji wa kanisa hili kama vile Raphael, Michelangelo na Gian Lorenzo Bernini.
Ujenzi wake uligharamia pesa nyingi. Wataalamu wengi huona ujenzi huu ulikuwa sababu moja ya Matengenezo ya Kiprotestanti yaani farakano na Kanisa Katoliki lililoanzia Ujerumani katika karne ya 16.
Ni kwamba Mapapa walianzisha kodi mpya kwa waumini ili waweze kuendeleza ujenzi. Madai ya pesa kwa ajili ya ujenzi huo yaliendeshwa kwa ukali uliosababisha upinzani wa Martin Luther na wengine hasa huko Ujerumani.
Kanisa hili lililojengwa juu ya eneo la mita za mraba 15,160 linaweza kupokea umati wa watu 60.000.
Lina urefu wa mita 211.5 na kimo cha mita 132.5.
Ukumbi wake una urefu wa mita 187 na upana wa 27.50. Ukumbi wa pili una urefu wa mita 138.
Jengo lina kuba moja kubwa na makuba manane ya kando.
Ndani ya kanisa kuna altare 45, nguzo 800, sanamu kubwa 390 za watu wa Biblia, Watakatifu na Mapapa.
This article uses material from the Wikipedia Kiswahili article Basilika la Mt. Petro, which is released under the Creative Commons Attribution-ShareAlike 3.0 license ("CC BY-SA 3.0"); additional terms may apply (view authors). Maudhui yanapatikana kwa chini ya CC BY-SA 4.0 isipokuwa iwe imebainishwa vinginevyo. Images, videos and audio are available under their respective licenses.
®Wikipedia is a registered trademark of the Wiki Foundation, Inc. Wiki Kiswahili (DUHOCTRUNGQUOC.VN) is an independent company and has no affiliation with Wiki Foundation.