Shuja (kwa maana „nyoka“, kwa Kilatini na Kiingereza Hydra) ni jina la kundinyota kubwa iliyopo upande wa kusini wa ikweta ya anga.
Kutokana na urefu wake Shuja inapakana na kundinyota nyingi ikiwa karibu na kundinyota za Zodiaki za Saratani (Cancer), Asadi (Leo) na Nadhifa (Virgo).
Shuja ilijulikana kwa jina hili kwa miaka mingi kati ya mabaharia Waswahili waliotumia nyota kutafuta njia baharini wakati wa usiku. Jina la Shuja limepokelewa kutoka kwa Waarabu wanaosema الشجاع ash-shujaaʿ kwa maana „nyoka“ na hapo walitafsiri jina la Wagiriki wa Kale walioona ama nyoka au joka na kumwita Ύδρα hidra, lililotafsiriwa kwa Kilatini kama "Hydra" ambalo ni sasa jina la kimataifa.
Katika mitholojia ya Kigiriki kuna hadithi mbili kuhusu Hydra; alikuwa joka mwenye vichwa vingi aliyekaa katika kinamasi na kumeza watu waliopita; nusu mungu Herakles alipambana naye lakini aliona ya kwamba akikata kichwa kimoja kiliota upya. Hapa alipata msaada wa kijana aliyewasha moto na kuchoma mashingo kila baada ya kukata kichwa kimoja.
Hadithi nyingine ya Wagiriki kuhusu nyota hizi ilitaja nyoka katika masimulizi ya Mungu Apollo na kunguru Ghurabu. Mungu Apollo alimtuma ndege wa kunguru (Ghurabu) kumchukulia maji kwa bakuli lakini ndege alichelewa kwa sababu alikula matunda njiani. Aliporudi akaeleza kuchelewa kwake kwa uwongo ya kuwa nyoka alimzuia akamwonyesha nyoka kwa kuishika kwenye miguu yake. Apollo alijua ni uwongo akakasirika na kumrusha kunguru (Ghurabu) pamoja na bakuli (Batiya-Crater) na nyoka (Shuja-Hydra) kwenye anga wanapokaa kama nyota.
Shuja ni kati ya kundinyota 48 zilizotajwa tayari na Klaudio Ptolemaio katika karne ya 2 BK. Lipo pia katika orodha ya kundinyota 88 zinazoorodheshwa na Umoja wa Kimataifa wa Astronomia kwa jina la Hydra. Kifupi chake rasmi kufuatana na Ukia ni 'Hya'.
Nyota za Shuja ni dhaifu kiasi kuna moja pekee ambayo ni angavu na hii ni Faridi (Alphard). Ina mwangaza unaonekana wa mag 2.0. Jina lake lamaanisha „Kipweke“ kwa Kiarabu yaani الفرد (al-fard) kwa sababu ni nyota angavu ya pekee, hakuna nyingine jirani nayo iliyopo angani. ,
Lane, Edward William: Arabic-English Lexicon (London: Willams & Norgate 1863), online hapa http://www.tyndalearchive.com/tabs/lane/
This article uses material from the Wikipedia Kiswahili article Shuja (kundinyota), which is released under the Creative Commons Attribution-ShareAlike 3.0 license ("CC BY-SA 3.0"); additional terms may apply (view authors). Maudhui yanapatikana kwa chini ya CC BY-SA 4.0 isipokuwa iwe imebainishwa vinginevyo. Images, videos and audio are available under their respective licenses.
®Wikipedia is a registered trademark of the Wiki Foundation, Inc. Wiki Kiswahili (DUHOCTRUNGQUOC.VN) is an independent company and has no affiliation with Wiki Foundation.