Mzungu ni neno la Kiswahili kumtaja mtu anayeonekana ametoka Ulaya.
Ni neno ambalo zaidi linalenga rangi ya mtu na kumtofautisha yule anayetajwa na Mwafrika, Mwarabu, Mhindi au Mchina.
Si neno kamili sana kwa sababu watu wanaoitwa Wazungu wanaweza kutokea kila sehemu ya dunia; Wamarekani weupe huitwa Wazungu na pia makaburu kutoka Afrika Kusini, Wakenya weupe na pia Waaustralia. Vilevile mtu kutoka nchi za Ulaya ya Kusini kama Hispania au Ugiriki anaweza kusababisha wasiwasi kama yeye ni Mzungu au Mwarabu kwa sababu wengi wao hufanana na watu wa Afrika ya Kaskazini.
Ikitumiwa kwa maana ya "watu wa Ulaya" inaeleweka kwa jumla isipokuwa siku hizi nchi za Ulaya hujaa watu ambao wenyewe au mababu wao walihamia huko kutoka pande nyingi za dunia jinsi inavyoonekana kwenye nyuso yao.
Kiasili neno lilijitokeza wakati ambako watu waliweza kuamini ya kwamba kila sehemu ya dunia ilikuwa na rangi yake. Kwa namna hiyo inafanana na maneno katika lugha nyingine kwa mfano "negroe/negre/Neger" katika lugha za Ulaya kwa watu wanaoonekana kama wenye asili ya Kiafrika. Haina dharau ndani yake kama neno la Kiarabu "abdi" linalotaja watu weusi pamoja na watumwa.
Neno "Kizungu" latumiwa mara nyingi kwa maana ya lugha ya Kiingereza, lakini wakati wa ukoloni wa Ujerumani katika Tanzania bara ("Afrika ya Mashariki ya Kijerumani") lilitaja pia Kijerumani.
Asili ya neno haijulikani kikamilifu.
Inaonekana kuna uhusiano na neno mzungu / mizungu lisilo kawaida tena katika Kiswahili cha kisasa lakini limetunzwa katika kamusi za Kiswahili zilizokusanya maneno yake mnamo mwaka 1900. Lilimaanisha mambo mbalimbali kama vile: 1) kitu cha ajabu au cha kushangaza, 2) mbinu ya kujiondoa katika tatizo, 3) aina ya muhogo, 4) silika au akili ya wanyama.
Waswahili waliwahi kutumia neno "mzungu" kwa "akili" na pia kwa mafundisho ya "unyago" yaliyoitwa "kufundishwa mizungu".. Kama asili ya "Wazungu" iko hapa iliweza kumaanisha "watu wa ajabu, wasio kawaida, wenye mbinu nyingi" au "wageni walio tofauti sana".
Wengine wamehisi kwa utani ya kwamba kuna uhusiano na kitenzi "kuzunguka" na "mzungu" ilitaka kutaja tabia ya wapelelezi, wamisionari na wafanyabiashara wa kwanza kutoka Ulaya ambao hawakukaa mahali pamoja bali walizungukazunguka kote Afrika.
This article uses material from the Wikipedia Kiswahili article Mzungu, which is released under the Creative Commons Attribution-ShareAlike 3.0 license ("CC BY-SA 3.0"); additional terms may apply (view authors). Maudhui yanapatikana kwa chini ya CC BY-SA 4.0 isipokuwa iwe imebainishwa vinginevyo. Images, videos and audio are available under their respective licenses.
®Wikipedia is a registered trademark of the Wiki Foundation, Inc. Wiki Kiswahili (DUHOCTRUNGQUOC.VN) is an independent company and has no affiliation with Wiki Foundation.